NEWS

Monday, 9 March 2026

Tarime: Barrick waokoa watu 22 waliozingirwa na mafuriko



Shughuli za uokoaji wakulima waliozingirwa na mafuriko katika eleo la Mashambani kijijini Matongo.

Na Mwandishi Wetu, Tarime

Kikosi cha Dharura na Uokoaji (ERT) kutoka Mgodi wa Dhahabu wa Barrick North Mara kimesaidia kuokoa watu 22 wakiwemo watoto - waliokuwa wamekwama kwa kuzingirwa na mafuriko katika kijiji cha Matongo, wilayani Tarime.

Wananchi hao ambao walikuwa wamepiga makambi kwa ajili ya kuvuna mazao yao katika eneo la Mashambani, walizingirwa na maji gafla na kulazimika kupanda juu ya miti ili kunusuru maisha yao, kwa mujibu wa Mkuu wa Wilaya ya Tarime, Meja Edward Gowele.

“Tulijitahidi kuokoa maisha yao wote waliokuwa wamezingirwa na maji na hakuna kifo wala majeruhi. Kwa hivyo, lazima tuwashukuru watu wa mgodi walifanya kazi kubwa kwa kushirikiana na timu ya uokoaji ya wilaya na mkoa,” Meja Gowele aliwambia waandishi wa habari jana.

Alifafanua kuwa kikosi cha uokoaji kutoka mgodi huo ambao unaendeshwa na kampuni ya Barrick kwa ubia na Serikali ya Tanzania kupitia kampuni ya Twiga Minerals kilitangulia kwenye eneo la tukio mara baada ya kupata taarifa - kikiwa na boti, magari na vifaa vingine vya kisasa vya uokoaji.
Shughuli za uokoaji zilianza Jumamosi iliyopita saa moja asubuhi hadi saa 12 jioni katika eneo hilo la Mashambani lenye makambi ya wakulima na wafugaji.

“Mimi mwenyewe nilikuwepo tangu mwanzo hadi mwisho na Kamati ya Usalama, pamoja na timu za uokoaji za wilaya na mkoa zikishirikiana na mgodi ambao walitusaidia kwa kutoa vifaa vya kisasa kwa ajili ya uokoaji. Kwa hivyo, tuna kila sababu ya kuwashukuru watu wa mgodi kwa kazi waliyofanya,” alisema Meja Gowele.

Baada ya kuokolewa, wananchi hao walipatiwa huduma ya kwanza na kusaidiwa kurejea kwenye makazi yao katika vijiji mbalimbali wilayani Tarime.

“Baada ya kuwatoa tuliwacheki kuona kama wanahitaji matibabu lakini wengi walikuwa wana njaa na niliagiza wakapata uji na maji,” alisema Mkuu wa Wilaya, Meja Gowele.

Mwenyekiti wa Serikali ya Kijiji cha Matongo, Charles Ryoba, alimshukuru Mkuu wa Wilaya, Gowele na Mgodi wa Barrick North Mara kwa kuchukua hatua za haraka kuokoa watu hao baada ya kuwapa taarifa za tukio hilo.

“Tunapenda kutoa shukrani za dhati kwa Mgodi wa Barrick North Mara kwa namna walivyopokea jambo hii na kufika kwa muda muafaka, hii inadhirisha wazi kuwa mahusinao yetu na Barrick ni mazuri,” alisema Ryoba mara baada ya shughulli za uokoaji kukamilika.
Ryoba alizishukuru pia timu za uokoaji za wilaya ya Tarime na mkoa wa Mara kwa kujitokeza kushiriki kuokoa maisha ya wananchi hao bila kukata tamaa.

“Mkuu wa Wilaya wetu alishinda site (eneo la tukio) tangu asubuhi hadi alipothibitisha kuwa watu wote wameokolewa. Nawashukuru pia wataalamu wote wa timu za uokoaji kutoka wilayani na mkoani,” alisema Mwenyekiti huyo wa Serikali ya Kijijji cha Matongo.
Eneo la Mashambani kijijini Matongo lipo jirani na Mto Mara ambao unatiririsha maji kwenye Ziwa Victoria upande wa Tanzania.

Mkuu wa Wilaya, Meja Gowele, alitumia nafasi hiyo pia kutoa wito wa kuwataka wananchi kuhama kutoka mabondeni, hasa misimu ya mvua nyingi.

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages