NEWS

Sunday, 8 March 2026

Liverpool FC Foundation yatembelea mradi wa ‘Save Her Seat’ Serengeti



Ujumbe kutoka Liverpool FC Foundation ukikabidhi zawadi ya vifaa vya michezo kwa wanafunzi walioshiriki tamasha hilo wilayani Serengeti.

Na Joseph Maunya
Serengeti
-----------------

Ujumbe kutoka Liverpool Football Club Foundation ya nchini Uingereza inayofadhili mradi wa ‘Save Her Seat’ umefika katika wilaya ya Serengeti na kujionea maendeleo ya utekelezaji wa mradi huo.

Mradi huo unatekelezwa kwa ushirikiano wa Kanisa la AICT Dayosisi ya Mara na Ukerewe na Shirika la Kimataifa la Right to Play mkoani Mara.
Ujumbe wa Liverpool Football Club Foundation ambao uliongozwa na Mkurugenzi wa Uendeshaji, Colin Contini na mshambuliaji wa zamani wa timu ya Wanawake ya Liverpool FC, Natasha Dowie, ulishuhudia na kushiriki michezo mbalimbali wakati wa tamasha la michezo la kuhamasisha umuhimu wa elimu kwa mtoto wa kike.


Natasha akishiriki mchezo wa mpira wa miguu wakati wa tamasha hilo

Tamasha hilo la michezo lilifanyika Machi 5, 2026 kwenye viwanja vya Shule ya Msingi Natta-Bigo iliyopo kata ya Natta wilayani Serengeti.

"Tunachofanya sisi (Liverpool FC Foundation) na Right to Play ni kuleta watu pamoja kupitia michezo ili kujifunza na kushiriki mapambano ya kuleta usawa wa kijamii, na kwa kweli tumefurahi sana kuwepo maeneo haya na tumeona watu wa jamii ya Natta ni wazuri na wakarimu sana," alisema Colin.

Naye Natasha alisema "Tumeona wanawake wengi wa Kiafrika wenye mafanikio makubwa kama wanasheria na wanamichezo pia, kwa hiyo kupitia hii michezo mabinti wadogo wanajenga umoja na kuhamasika kutokatia tamaa ndoto zao hata kama wanakumbana na mazingira magumu kiasi gani."


Natasha akizungumza katika tamasha hilo

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Miradi kutoka AICT Dayosisi ya Mara na Ukerewe, Charles Mashauri, aliishukuru Liverpool FC Foundation kwa kufadhili mradi huo na kuiomba taasisi hiyo kuendelea kutoa msaada ili jamii iendelee kupata elimu zaidi.

"Tunawashukuru sana Liverpool FC Foundation kwa kutoa michango na kutuwezesha kuendeleza shughuli hii ya kutoa elimu kwa jamii juu ya vikwazo mbalimbali vinavyomzuia mtoto wa kike kupata elimu na tunaomba waendelee bila kuchoka," alisema Mashauri.


Mashauri akizungumza katika tamasha hilo

Akizungumza kwa niaba ya wanajamii wa Natta, Avelina Masota Mwengi, naye aliishukuru taasisi hiyo kwa kufadhili AICT na Right to Play ili kusaidia kuhamasisha jamii kuachana na mila kandamizi kwa watoto wa kike kama vile ukeketaji na ndoa za utotoni.

AICT na Right to Play zimekuwa zikishirikiana kutekeleza mradi wa Save Her Seat kwa ufadhili wa Liverpool FC Foundation kwa lengo la kusaidia watoto wa kike katika wilaya za Serengeti na Tarime, mkoani Mara kupata ujuzi utakaowasaidia kukabiliana na vikwazo vya kupata elimu.


Wasanii wa ngoma ya asili wakionesha umahiri wao katika tamasha hilo

Chanzo: Gazeti la Sauti ya Mara

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages