NEWS

Tuesday, 21 April 2026

TRA Mara yaanza kutoa elimu kwa wananchi kuhusu masuala ya forodha



Maafisa wa TRA Mkoa wa Mara wakijitambulisha kwa Mkuu wa Wilaya ya Tarime, Meja Edward Gowele, kabla ya kwenda kuelimisha kuhusu masuala ya forodha jana.

Na Mwandishi Wetu
Tarime
--------------

Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) Mkoa wa Mara imeanza kutoa elimu kwa wananchi wa wilayani Tarime kuhusu mambo ya forodha, hususan uingizaji na uondoaji bidhaa nchini.

Kabla ya kwenda kuanza utoaji wa elimu hiyo, maafisa hao wa TRA walikwenda kujitambulisha kwa Mkuu wa Wilaya ya Tarime, Meja Edward Gowele, ambaye aliwapongeza kwa jitihada hizo za kutoa elimu kwa wananchi kuhusu masuala ya biashara na ulipaji wa kodi.

Meja Gowele alisema wafanyabiashara wanaoingiza na kutoa bidhaa nchini wana nafasi kubwa ya kuchangia mapato ya serikali iwapo watazingatia taratibu na sheria zilizowekwa kwa maendeleo ya taifa.

“Nawashukuru kwa jambo hili jema la kutoa elimu kwa wananchi wetu, hasa kwa wafanyabiashara wanaoingiza na kutoa bidhaa nchini. Kama kila mwananchi atazingatia, naamini tutaongeza mapato makubwa kwa ajili ya mambo ya msingi ya nchi yetu,” alisema.

Elimu hiyo ambayo inagusa taratibu na sheria za forodha, ilianza kutolewa jana Aprili 20, 2026 kwa wananchi wanaoishi katika mji wa Sirari uliopo mpakani na nchi ya Kenya.

Walengwa wa elimu hiyo ni wananchi wa kawaida na wafanyabiashara wa wilaya ya Tarime.
Afisa Elimu na Mawasiliano kwa Umma wa TRA, Ruekaza Rwagoshora, alionya kuwa kupitisha mzigo nje ya kituo cha forodha kunalinyima taifa mapato yake na nchi inakosa taarifa muhimu kuhusu jinsi biashara inavyofanyika.

Naye Afisa wa TRA wa Kitengo cha Wateja, Emmanuel Grayson Muchunguzi, alisema serikali imeanza kuondoa ushuru kwa pembejeo zinazoagizwa kutoka nje ya nchi.

"Njoo ofisi za forodha tutakupa kibali cha kuleta mbolea," Muchunguzi aliwambia wananchi na kuongeza kuwa wafanyabiashara wadogo wafike ofisi za forodha na kufanyiwa tathmini na kulipa ushuru unaoendana na mizigo yao.
Kwa wafanyabiashara wakubwa, aliwataka wafike ofisi za forodha na waagize bidhaa kwa kuwatumia mawakala wa forodha moja kwa moja kutoka kiwandani.
Baadhi ya wananchi walitaka huduma za forodha zisogezwe karibu na sehemu wanapoishi.

TRA kupitia Kituo cha Forodha Sirari inalenga kufikisha elimu hiyo katika maeneo yote yenye shughuli za kibiashara wilayani Tarime.
(Picha zote na Mara Online News)

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages