
Askofu wa Kanisa Katoliki Jimbo la Musoma, Michael Msonganzila, akiwapongeza Mama Leah (kulia) na Anita Gimero Waitara (katikati) kwa michango waliyotoa katika harambee ya kuchangia ujenzi wa kanisa jipya la Parokia ya Nyamwaga jana Jumapili. Kushoto ni Paroko wa Parokia hiyo, Padre Julius Manyonyi.
Tarime
------------
Shilingi milioni 259 zimechangwa katika harambee ya kuendeleza ujenzi wa jengo jipya la Kanisa Katoliki la Mt. Mathayo Mwinjili, Parokia ya Nyamwaga, wilayani Tarime, Mara.
Harambee hiyo ilifanyika katika viwanja vya kiinjili Keisangora - Nyamwaga jana Jumapili, ikiongozwa na mdau wa maendeleo Anitha Gimero Waitara.
Anita akichangisha fedha katika harambee hiyo
Miongoni mwa wadau wengine wa maendeleo waliopiga jeki harambee hiyo ni mfanyabishara maarufu wa mjini Tarime, Mama Leah (Agnes Mwita Chacha), Mkurugenzi wa Goldland Hotel, Simon Mseti Wangwe na Mkurugenzi wa Kampuni ya Rubida, Chacha Ernest Mwera, ambao kila mmoja alichangia shilingi milioni 10.
Mmoja wa familia ya wachimbaji madini kutoka Buhemba akizungumza katika harambee hiyo
Akizungumza katika harambee hiyo, Anita ambaye pia ni mzaliwa wa kijiji cha Nyankoni wilayani Tarime na Mkurugenzi wa Kampuni ya Gimero & Sons Ltd, alionesha matumani makubwa kwamba ujenzi wa jengo la kanisa hilo utakamilika.
“Mimi binti yenu (msubati) ninapenda kuwambia kanisa hili litaezekwa na kukamilika kabla ya miaka sita iliyopagwa,” alisema Anita mbele ya mamia ya wageni na waumini wa Parokia ya Nyamwaga.
Anita (kushoto) na Mama Leah wakipongezana wakati wa harambee hiyo
“Namshukuru sana Mama Leah na Simon Mseti Wangwe. Pia, nimefarijika sana kwa michango ya familia ya wajimbaji madini na wengine wote, mbarikiwe sana,” alisema Anita.
Mhashamu Askofu Msonganzila akimkabidhi Simon Mseti Wangwe zawadi ya kitambaa cha suti wakati wa harambee hiyo.
Desemba 2023, Anita alishiriki harambee ya kanisa hilo na kutoa fedha kwa jili ya ununuzi wa mabati yote ya kuezeka jengo hilo, lakini zikaelekezwa kwenye shughuli nyingine za ujenzi huo.
“Niliahidi kuezeka kanisa na kutoa mabati yote, lakini pesa ikaelekezwa kwa kazi nyingine, ndio maana Baba Askofu ameridhia mimi nirudi kuchangia. Nasikia faraja sana kuja katika harambee hii ya kuezeka kanisa hii.
“Fr. Paroko, umeniheshimisha nyumbani kwa kuniombea kwa Askofu kuja hapa, hakika nimeuona mkono wa bwana,” alisema Anita.

Simion Kilesi akikabidhi mchango wake wa shilingi milioni mbili.
Kwa upande wake Mhashamu Askofu Msonganzila naye aliwashukuru wadau mbalimbali kwa kuendelea kujitoa kwa hali na mali kwa ajili ujenzi wa kanisa la parokia hiyo.
Awali, kiongozi huyo wa kiroho aliwakumbusha waamini na wageni wote waliohudhuria harambee hiyo kuendelea kuwa watu wema na kufanya kazi ya Mungu.

Chacha Ernest Mwera (aliyeshika kipaza sauti) akizungumza mara baada ya kukabidhi mchango wake wa shilingi milioni 10.
Ujenzi wa jengo hilo litakalokuwa na uwezo wa kutumiwa na watu 1,500 kwa wakati mmoja, unatarajia kugharimu shilingi zaidi ya bilioni mbili.
Nao waamini wa kanisa hilo walimshukuru Anitha na wadau wengine kwa kuendelea kuchangia ujenzi wa kanisa hilo.
“Tunamshukuru Mungu harambee imeenda vizuri, tumepata michango mizuri, tutapiga hatua kwenye ujenzi wa kanisa letu,” alisema mmoja wa waumini wa kanisa hilo.





No comments:
Post a Comment