NEWS

Friday, 6 September 2024

Mapambano dhidi ya ukatili kwa watoto: Shirika la WiLDAF lawajengea walimu uwezo



Sehemu ya walimu wakiwa katika mafunzo ya kujengewa uwezo wa kupiga vita ukatili dhidi ya watoto yanayoendeshwa na Shirika la WiLDAF Tanzania mjini Tarime leo.
---------------------------------------------

Na Mwandishi Wetu/ Mara Online News

Shirika la Wanawake katika Sheria na Maendeleo Afrika (WiLDAF) Tanzania kupitia mradi wake wa Jamii Imara, limeendesha mafunzo kwa walezi wa klabu za shule salama, sambamba na elimu ya ujasiriamali kwa wanawake wilayani Tarime.

Mafunzo hayo ya siku mbili yanahitimishwa mjini Tarime leo Septemba 6, 2024 kwa walimu walezi wa klabu hizo, na baadhi ya wanawake kutoka kata za Komaswa na Regicheri.

Mwezeshaji wa mafunzo kwa walimu hao, Thomas Diwani Mponda amesema wanajengewa uwezo wa kuelimisha wanafunzi maana ya ukatili, vyanzo vyake, madhara yake, namna ya kuripoti na wapi pa kuripoti taarifa za vitendo hivyo.

Mwezeshaji Thomas Diwani Mponda 
akizungumza katika mafunzo hayo.
---------------------------------------------


Kwa mujibu wa Afisa Mradi wa WiLDAF Tanzania, Suzan Kawanga, shirika hilo chini ya ufadhili kutoka Ubalozi wa Marekani, limeanzisha klabu za shule salama katika baadhi ya shule za msingi na sekondari katika wilaya za Butiama, Serengeti na Tarime mkoani Mara.

“Kupitia mradi wetu wa Jamii Imara, tumefanikiwa kuanzisha klabu hizo kwenye shule mbili za msingi na moja ya sekondari katika kila wilaya,” Kawanga amefafanua.

Kwa upande wake Mwalimu Maseke Bisansaba kutoka Shule ya Msingi Komaswa amesema mafunzo hayo yatasaidia kupunguza vitendo vya ukatili wa kijinsia ukiwemo ukeketaji kwa wasichana.

Kuhusu mafunzo ya ujasiriamali kwa wanawake, Kawanga amesema lengo ni kuwajengea uwezo wa kuendesha miradi ya kiuchumi ili kujiongezea kipato.

Sehemu ya wanawake wakishiriki 
mafunzo hayo ya ujasiriamali.
------------------------------------------

“Wanawake wanapokuwa vizuri kiuchumi wanaweza kutunza watoto wao na kuwalinda dhidi ya vitendo vya ukatili,” amesema Afisa Mradi huyo wa Shirika la WiLDAF.

Afisa Mtendaji wa Kata ya Komaswa, Joyce Mbusi na mjasiriamali Anna Ndera kutoka kata ya Regicheri wamesema mafunzo hayo ni chachu ya kuwakomboa wanamke kiuchumi ili kupunguza utegemezi na kuboresha maisha yao.
Read Also Section Example

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages