
Wansato Marwa Wambura enzi za uhai
Na Mwandishi Wetu
Kundi la watu kadhaa wanaodaiwa kuwa Kipsigis kutoka Transmara Kusini nchini Kenya, limemshambulia hadi kumuua raia wa Tanzania, Wansato Marwa Wambura, mkazi wa kijiji cha Mangucha, kata ya Nyanungu wilayani Tarime.
Viongozi wa kata ya Nyanungu na serikali ya kijiji cha Mangucha wamethibitisha kutokea kwa tukio hilo.
Kwa mujibu wa Afisa Mtendaji wa Serikali ya Kijiji cha Mangucha, John Masero, Wansato alishambuliwa kwa mishale na panga Ijumaa iliyopita saa saba mchana wakati akichunga mifugo yake katika eneo la Nyanderema mpakani mwa Kenya na Tanzania.
"Alifariki majira ya saa 11 za jioni siku hiyo hiyo akiwa katika kituo cha afya Masanga,” alisema Masero.
Diwani wa Kata ya Nyanungu, Tiboche Richard alilaani tukio hilo na kuliita la kinyama.
“Kwa kweli tumepoteza ndugu, rafiki na kaka yetu Wansato Wambura kwa kushambuliwa na majirani zetu akiwa malishoni. Hivyo niwaombe wananchi wetu kuendelea kuwa watulivu katika kipindi hiki kigumu,” Diwani huyo kutoka chama tawala - CCM aliandika kwenye mtandao wa kijamii.
Taarifa zaidi zinasema marehemu huyo atazikwa leo Jumatatu kijijini Mangucha.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Polisi Tarime Rorya hakupatikana mara moja kuzungumzia tukio hilo.
UNAWEZA PIA KUSOMA:
>>BoT yapata mafanikio makubwa ununuzi wa dhahabu safi kuimarisha akiba ya fedha za kigeni nchini
>>Majaliwa awatembelea majeruhi Muhimbili
>>TANAPA, KfW wajenga bweni la wasichana Sekondari ya Manchira kwa gharama ya shilingi milioni 334
>>PSSSF yalipa trilioni 10.46 kwa wanufaika zaidi ya 300,000 tangu ianzishwe miaka 6 iliyopita
No comments:
Post a Comment