
Na Mwandishi Wetu
Kesho Jumatatu ya Julai 28, 2025 ni siku ya kipekee iliyobeba ndoto za watia nia wa nafasi za ubunge na udiwani kote nchini, ambapo Chama Cha Mapinduzi (CCM) kinatarajiwa kuanza kuweka hadharani orodha ya majina ya waliopenya hatua ya kwanza ya mchujo na kurejeshwa majimboni kwa ajili ya kuchuana kwenye kura za maoni.
Joto la kisiasa ni kali - na bila shaka katika kila kona ya nchi gumzo ni moja tu: “Nani karudi? Nani kakatwa?” Wajumbe wa kura za maoni majimboni nao wamejaa hamasa, wakiwa wamejiandaa kufanya maamuzi magumu.
Ni siku ya hofu kwa baadhi, siku ya ushindi wa awali kwa wengine, na kwa CCM ni siku ya kuonesha umakini wake katika kuleta timu ya watia nia imara, ambao baadaye miongoni mwao watateuliwa kupeperusha bendera ya chama hicho tawala katika Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 29, 2025.
Inaelezwa kuwa vikao vya maamuzi vya CCM ngazi ya taifa vinavyoendelea jijini Dodoma vinapitia kwa kina na umakini mkubwa majina ya watia nia, huku vigezo vya uadilifu, rekodi ya utendaji na uwezo wa kuunganisha jamii vikizingatiwa.
Kwa ujumla, wanachama wa CCM na Watanzania kwa ujumla wameelekeza macho na masikio yao Dodoma wakisubiri kwa shauku kubwa majina yaliyochomoza - mithili ya wanafunzi wanaosubiri matokeo ya mtihani wa kitaifa.
Unaweza pia kusoma:
»Ilani ya CCM 2020-2025 ilivyotekelezwa kwa mafanikio makubwa kata ya Rabuor wilayani Rorya chini ya uongozi wa Ng’ong’a
»TEKNOLOJIA:Wakurugenzi Mara wapokea kompyuta 142 kuimarisha mfumo wa kidijitali vituo vya huduma za afya
»MAKALA YA MAJI:Mradi wa bilioni 21/- kuboresha huduma ya maji mjini Mugumu, RC Mara amtaka mkandarasi kuukamilisha kwa wakati
No comments:
Post a Comment