
Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa 2025, Ismail Ali Ussi, akizindua upanuzi mradi wa chanzo cha maji unaotekelezwa kutokana na fedha za CSR Barrick North Mara leo Agosti 21. Wa kwanza kushoto ni Mkuu wa Wilaya ya Tarime, Meja Edward Gowele na katikati ni Meneja Mkuu wa Mgodi wa North Mara, Apolinary Lyambiko.
-------------------------------------
Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa 2025, Ismail Ali Ussi, leo Agosti 21 amezindua mradi wa upanuzi wa chanzo cha maji kilichopo Mgodi wa Dhahabu wa North Mara kwa ajili ya kuhudumia wakazi wa vijiji saba zaidi vinavyozunguka mgodi huo katika Halmashauri ya Wilaya ya Tarime, mkoani Mara.
Mradi huo unatekelezwa kwa gharama ya shilingi bilioni 2.665 za Uwajibikaji wa Kampuni kwa Jamii (CSR) zilizotolewa na mgodi huo - unaoendeshwa na Kampuni ya Barrick kwa ubia na Serikali ya Tanzania kupitia Kampuni ya Twiga Minerals.
Akizungumza baada ya kukagua na kuzindua mradi huo unaolenga pia kupeleka maji katika kijiji jirani cha Kewanja, Ussi ameipongeza Barrick kwa jinsi inavyojali huduma bora za kijamii na maendeleo ya wananchi.
“Kwa dhati ya moyo wangu ninamshukuru na kumpongeza sana mwekezaji huyu [Barrick] - ana dhamira ya kuhakikisha taifa letu linapata maendeleo,” amesema na kuitaja kampuni hiyo kuwa ni miongoni mwa wawekezaji wa kigeni wanaofanya vizuri nchini.

Aidha, Ussi ameipongeza Wakala wa Maji na Usafi wa Mazingira Vijijini (RUWASA) Mkoa wa Mara kutokana na usimamizi mzuri wa utekelezaji wa miradi ya maji.
“Hatukuona changamoto yoyote ya miradi ya maji tangu tuingie katika mkoa huu - na tumeridhika kwa asilimia 100 juu ya utekelezaji wa miradi hii,” amesema Ussi.
Ussi ametumia nafasi hiyo pia kumpongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kujenga mazingira bora ya uwekezaji nchini.


Awali, Kaimu Meneja wa RUWASA Wilaya ya Tarime, Mhandisi Mohamed Mtopa, amemweleza kiongozi huyo wa mbio za mwenge kwamba mwanzoni chanzo hicho cha maji kilisanifiwa kuhudumia wakazi 27,742 wa vijiji vinne vya Nyangoto, Matongo, Mjini Kati na Nyabichune.
Lakini kutokana na ongezeko la mahitaji ya maji katika vijiji saba vinavyozunguka mgodi wa North Mara, chanzo hicho kilisanifiwa upya kwa lengo la kuhudumia wakazi 125,566 katika vijijni sita vya Genkuru, Nyamwaga, Nyakunguru, Kerende, Msege na Komarera.
Kwa mujibu wa Mhandisi Mtopa, mradi huo ambao utekelezaji wake umefikia asilimia 80, utaongeza uzalishaji kutoka lita 2,314,000 za sasa hadi 10,213,000 na hivyo kufikia lengo la serikali la mwaka 2020-2025 la upatikanaji wa maji safi na salama kwa wananchi waishio vijijini.
Mradi huo unatarajiwa kuwaondolea wakazi wa vijiji husika adha waliyokuwa nayo ya kutumia muda mrefu kutafuta maji, ambapo sasa watapata muda wa kujielekeza kwenye shughuli za uzalishani mali na kukuza uchumi wao.
Mapema, pamoja na miradi mingine, Kiongozi wa Mbio za Mwenge, Ussi, amezindua zahanati ya kijiji cha Mangucha katika Halmashauri ya Wilaya ya Tarime - ambacho pia kimejenggwa kutokana na fedha za CSR Barrick North Mara.
No comments:
Post a Comment