NEWS

Friday, 12 September 2025

Timu ya TEITI yazuru Barrick North Mara kutathmini miradi ya CSR, ‘local content’



Watalaamu kutoka TEITI wakiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya maafisa waandimizi wa Mgodi wa Dhahabu wa Barrick North Mara walipofanya ziara katika mgodi huo jana Septemba 11, 2025.

Na Mwandishi Wetu, Tarime

Timu ya wataalamu wa Taasisi ya Uhamasishaji Uwazi na Uwajibikali katika Rasilimali za Madini, Mafuta na Gesi Asilia (TEITI) ilitembelea Mgodi wa Dhahabu wa North Mara jana Septemba 11, 2025 kujionea mchango wake kwa maendeleo ya kijamii na kiuchumi.

Eneo kubwa lililopewa kipaumbele katika ziara ya wataalamu hao ni Uwajibikaji wa Kamupuni kwa Jamii (CSR) na ushirikishwaji wa Watanzania (local content).


Kiongozi wa msafara wa wataalamu kutoka TEITI, Andrew Eriyo (wa pili kulia), wakitembelea miradi inayotekelezwa chini ya mpango wa CSR wa Mgodi wa Barrick North Mara jana. Wa pili kutoka kushoto ni Meneja Mahusiano wa Mgodi huo, Francis Uhadi na wa kwanza kulia ni Mwanasheria wa TEITI, Julieth Moshi.

Msafara wa wataalamu hao uliongozwa na Mkuu wa Sehemu ya Utafiti kutoka TEITI, Andrew Eriyo.

“Lengo kuu ni kutathmini utekelezaji wa sheria ya madini upande wa CSR na local content,” alisema Eriyo.

Meneja Mkuu wa Mgodi wa North Mara, Apolinary Lyambiko, aliwakaribisha wataalamu hao wa TEITI katika mgodi uliopo Halmashauri ya Wilaya ya Tarime, mkoani Mara.

“Karibuni sana, CSR ni suala la msingi, na tathmini kama hizi huwa zinasaidia sana kuboresha mambo kwenda vizuri zaidi,” alisema Lyambiko.


Meneja Mkuu wa Mgodi wa Barrick North Mara, Apolinary Lyambiko, akizungumza na watalaamu kutoka TEITI waliotembelea mgodi huo jana.


Timu ya watalaamu kutoka TEITI ikitembelea baadhi ya miradi ya CSR, ikiwemo ya elimu katika vijiji vilivyo jirani na mgodi wa North Mara jana.

Mgodi wa North Mara unatumia mabilioni ya fedha kugharimia miradi ya maendeleo katika vijiji vya Halmashauri ya Wilaya ya Tarime, huku suala la ‘local content’ nalo likipewa kipaumbele.

“Tuna miradi ambayo imekamilika na ambayo utekelezaji wake unaendelea. Mfano, kuna upanuzi wa mradi wa maji Nyangoto ambao ulitembelewa na Mwenge wa Uhuru hivi karibuni,” alisema Meneja Uhusiano wa Mgodi wa huo, Francis Uhadi.



Uhadi alitaja miradi mingine iliyokamilika kuwa ni pamoja na utengenezaji wa madawati zaidi ya 9,000 ambayo yamegawiwa kwenye shule za msingi na sekondari katika Halmashauri ya Wilaya ya Tarime kuunga mkono juhudi za serikali za kuboresha mazingira ya elimu.

Madawati hayo yamegharimu shilingi milioni 800 za CSR, Uhadi alisema.

“Tuna miradi mingine mingi ya CSR, ukiwemo ujenzi wa zahanati, vyumba vya wagonjwa wa nje, madarasa na hata uzio katika shule,” aliongeza Uhadi.


Kiongozi wa msafara wa wataalamu kutoka TEITI, Andrew Eriyo (wa pili kushoto), akijionea moja ya mazao yanayolimwa katika shamba darasa ambalo limeanzishwa na Mgodi wa North Mara kama sehemu ya juhudi za kuinua uchumi wa vijana katika kijiji cha Matongo, wilayani Tarime.

Kuhusu suala la ‘local content’, mgodi huo unatoa kipaumbele kwa wazawa kwenye suala la ajira na fursa za kibiashara kwa jamii zinazozunguka mgodi huo unaoendeshwa na kampuni ya Barrick kwa ubia na Serikali ya Tanzania kupitia kampuni tanzu ya Twiga Minerals.

“Mfano, tumeweka utaratibu wa kuhakikisha kuwa kazi zisizohitaji stadi zozote wanapewa watu waliopo maeneo jirani na mgodi,” Uhadi alieleza.

Ujumbe huo wa TEITI ulitembelea pia miradi mbalimbali inayotekelezwa kwa fedha za CSR na kuridhishwa na kazi nzuri inayofanywa na kampuni ya Barrick katika kuchangia maendeleo ya Watanzania.


Afisa Mchumi Mkuu kutoka TEITI, Tibenda Njoki, akisisitiza jambo katika ziara ya kutembelea mgodi wa North Mara.

“Mgodi wa Barrick North Mara umekuwa mdau wetu mkubwa na leo tumewatambelea kuangalia wanavyofanya kwenye eneo la CSR na local content,” alisema mmoja wa watalaamu hao kutoka TEITI, Anastazia Ryoba.

Mbali na North Mara, Kampuni ya Barrick pia inaendesha Mgodi wa Dhahabu wa Bulyanhulu ulioko wilaya ya Kahama, mkoani Shinyanga.

TEITI ni taasisi ya serikali inayohamasisha uwazi na uwajibikaji katika rasilimali za madini, mafuta na gesi asilia ili kuhakikisha mapato yanayotokana na rasilimali hizo yanakuwa na mchango mkubwa kwa maendeleo ya Watanzania na taifa kwa ujumla.
Read Also Section Example

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages