NEWS

Thursday, 31 October 2024

Kanisa la AICT, Right to Play waadhimisha Siku ya Mtoto wa Kike wakisisitiza haki ya elimu kwa wasichana



Viongozi wakikabidhi zawadi ya jezi kwa wanafunzi wakati wa tamasha la michezo lililoandaliwa na Kanisa la AICT na Shirika la Right to Play katika Shule ya Msingi Tumaini wilayani Serengeti juzi Oktoba29, 2024. Picha na Mara Online News)
-------------------------------------------

Na Godfrey Marwa, Serengeti

Kanisa la AICT Dayosisi ya Mara na Ukerewe kwa kushirikiana na Shirika la Right to Play wameadhimisha Siku ya Mtoto wa Kike Duniani kwa kuhamasisha jamii kuwapatia watoto wa kike haki ya kupata elimu.

Uhamasishaji huo ulifanyika juzi Oktoba 29, 2024 wakati wa tamasha la michezo kwa wanafunzi lililoandaliwa na taasisi hizo katika Shule ya Msingi Tumaini iliyopo wilaya ya Serengeti mkoani Mara.

Kaulimbiu ya tamasha hilo ambalo lilikuwa na lengo la kuelimisha jamii umuhimu wa elimu kwa mtoto wa kike inasema: "Mtoto wa Kike na Uongozi; Tumshirikishe Wakati ni Sasa."

Afisa Mradi wa Save Her Seat na Elimu Jumuishi kutoka AICT na Right to Play, Daniel Fungo alitoa wito wa kuhamasisha kila mmoja kuwa balozi wa kupiga vita vikwazo vya elimu kwa watoto wa kike.

"Tuwe mabalozi wa kutokomeza vitendo vinavyokwamisha mtoto wa kike kupata elimu. Watoto wa kike wakisoma wanasaidia kuliko wa kiume, hivyo wapatiwe fursa kusoma kama wa kiume," alisisitiza Fungo.

Mwanafunzi wa shule hiyo, Evaline Samson aliishukuru AICT na Right to Play kwa kuwapa elimu ya stadi za maisha kupitia mradi wa Save Her Seat.

Evaline Samson
----------------------


"Nimezielewa haki zangu, haki za mtoto za kuishi, kulindwa, kuendelezwa na kushirikishwa mambo yanayotuhusu watoto wa kike katika jamii," alisema Evaline.

Alisema wazazi kutozungumza na watoto ni changamoto kubwa. "Moja ya changamoto inayotukabili ni wazazi kukosa muda wa kuzungumza na sisi ili kujua changamoto tunazopitia," alisema.


Mwalimu Gladis Magati
-------------------------------


Naye Mwalimu Mlezi wa Klabu ya Mradi wa Save Her Seat katika Shule ya Msingi Tumaini, Gladis Magati alisema kwamba kupitia mradi huo wameweza kuwafundisha wanafunzi stadi za maisha, hivyo kuwajengea wanafunzi hali ya kujiamini na kuimarisha mahusiano mema baina yao.

Tamasha hilo lilihusisha michezo ya mpira wa miguu kwa wasichana na wavulana, mpira wa pete kwa wasichana, kukimbia kwenye gunia, ngonera, maigizo na kukimbia na chupa kichwani. Washindi walizawadiwa jezi na vinywaji baridi.
Read Also Section Example

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages